STRAIKA, Amissi Tambwe, wa Simba amefikisha mabao 19 katika Ligi
Kuu Bara baada ya jana Jumapili
kuiwezesha timu yake kushinda mabao 3-2 dhidi ya Ruvu Shooting, huku klabu ya DC Motema Pembe ya Jamhuri ya Kidemkrasia ya Congo, ikimpigia simu kutaka kumsajili haraka.
kuiwezesha timu yake kushinda mabao 3-2 dhidi ya Ruvu Shooting, huku klabu ya DC Motema Pembe ya Jamhuri ya Kidemkrasia ya Congo, ikimpigia simu kutaka kumsajili haraka.
Katika mchezo dhidi ya Ruvu Shooting uliofanyika
Uwanja wa Taifa, Tambwe ambaye ni raia wa Burundi, aliifungia Simba mara
mbili dakika za 23 na 33.
Bao la kwanza alilifunga akimalizia mpira
uliotemwa na kipa Abdallah Rashid wakati akiokoa shuti kali la Said
Ndemla. La pili alilifunga pale alipounganisha krosi safi ya Haroun
Chanongo.
Mabao hayo yanamfanya Tambwe kuvuka rekodi ya Boniface Ambani aliyefunga mabao 18 msimu wa 2010/11 alipokuwa Mfungaji Bora.
Bao la tatu la Simba katika mchezo huo
uliohudhuriwa na watazamaji wachache huku mvua ikitawala muda mwingi,
lilifungwa na Chanongo dakika ya 75 baada ya kupokea pasi ya Amri
Kiemba.
Ruvu Shooting ilipata bao la kwanza dakika ya 68
lililofungwa na Said Dilunga kwa kichwa akiunganisha kona ya Michael
Aidan. Bao la pili la Ruvu lilifungwa kwa njia ya penalti dakika ya 82
na Jerome Lembele.
Mwamuzi, Nathan Lazaro, wa Kilimanjaro alitoa
penalti hiyo baada ya beki wa Simba, Joseph Owino, kuunawa mpira ndani
ya eneo la hatari.
Licha ya ushindi huo, Simba imebaki katika nafasi
ya nne ikiwa na pointi 35 kwani Mbeya City ina pointi 36 katika nafasi
ya tatu baada ya juzi Jumamosi kutoka suluhu na Oljoro JKT.
Baada ya mchezo huo, Kocha wa Simba, Zdravko Logarusic alisema:
“Nimefurahi kupata ushindi huu, lakini nimefurahishwa zaidi na mabao tuliyofunga. Sasa naangalia michezo inayofuata.”
Naye Kocha wa Ruvu, Tom Olaba alisema: “Japokuwa
napoteza mechi pili mfululizo, nashukuru tumecheza na kupunguza idadi
ya mabao ya kufungwa sasa natengeneza timu ya msimu ujao.”
Wakati huohuo, DC Motema Pembe ya Jamhuri ya
Kidemokrasia ya Congo, imempigia simu Tambwe ikitaka kumsajili kwa msimu
ujao wa Ligi Kuu ya nchi hiyo.
Tambwe aliliambia Mwanaspoti kuwa viongozi wa Motema Pembe
walimpigia simu wakitaka ajiunge nao kwa msimu ujao na mazungumzo yao
yanaenda vizuri kwani kilichobaki ni klabu hiyo kumalizana na Simba kwa
kuwa bado ana mkataba na Wekundu wa Msimbazi hao.
“Nilipojiunga na Simba nilisaini mkataba wa miaka
miwili, mwishoni mwa msimu huu nitakuwa nimemaliza mwaka mmoja hivyo
Motema Pembe wanatakiwa kumalizana na Simba, mimi sina tatizo,” alisema
Tambwe.
“Malengo yangu ni kucheza soka la kimataifa zaidi,
sijaridhika na hapa nilipo, tayari ndoto zangu zimeanza kutimia
kutokana na Motema Pembe kuonyesha nia ya kunisajili.”