Monday, 3 March 2014

Yanga yashtukia uongo wa Al Ahly

Kocha Mkuu wa Yanga, Hans van Der Pluijm.
Na Hans Mloli
KOCHA Mkuu wa Yanga, Hans van Der Pluijm, amewashtukia Al Ahly na kukiri kwamba waliwadanganya Yanga kwa kudai watakuja na winga wao Emad Motaeb, lakini haikuwa hivyo.
Al Ahly ilitoa taarifa mbalimbali kwenye vyombo vya habari vya Cairo kwamba itatua na winga wao hatari Motaeb jijini Dar es Salaam kwa ajili ya mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Yanga lakini haikuwa hivyo.

Pluijm amecharuka na kusema anajua kwamba, Ahly walitangaza kuja na winga huyo ili kuwatisha Yanga, lakini wameamua kumuacha kwa ajili ya mchezo wa marudiano utakaochezwa Jumapili ijayo kwa kuwa wameweka nguvu zaidi kwenye mchezo huo wa pili.
Hata hivyo, Pluijm ameliambia Championi Jumatatu kuwa, hawajatishika na hilo na kikosi chake kinajiandaa kwenda Misri kupambana ili kuibuka na ushindi.
Ingawa Pluijm amekiri kwamba Motaeb ni hatari na ni mwepesi anapokuwa uwanjani linapofika suala la kushambulia.
“Wale ni wajanja, nazijua mbinu zao, huenda wakabadilika kwenye mchezo wa marejeano, inabidi kujiandaa kwa kila kitu kwa sababu sidhani kama watacheza hivi kwa staili hii waliyoitumia leo.
“Hata hivyo, kuna mchezaji mmoja sijamuona na yupo kwenye timu yao, ni hatari sana, mara nyingi huwa anacheza winga, simjui jina lake sawasawa, najaribu kulikumbuka jina lake lakini linanitoka ila namfahamu kwa staili yake ya uchezaji,” alisema Pluijm na kuongeza:
“Hata hivyo haimaanishi kwamba tukienda kule tutazuia tu, hapana tutacheza kwa kushambulia kwa sababu tunahitaji ushindi, bado tunahitaji mabao kwa ajili ya kujihakikishia kuvuka raundi hii.”
Uchunguzi uliofanywa na Championi Jumatatu umegundua kuwa mchezaji aliyesemwa na Pluijm ni Motaeb ambaye ni mmoja wa wachezaji hatari kwenye kikosi cha Al Ahly na huvaa jezi namba tisa mgongoni.
Mbinu nyingine iliyoonekana kutumika na Waarabu hao ni ile ya kumbadili namba mchezaji wao, Sayed Abdel Wahed ambaye hutumika kwenye nafasi ya kiungo mshambuliaji lakini juzi alionekana kupewa majukumu ya beki wa kushoto.
Yanga itakwenda Misri kurudiana na Al Ahly Jumapili ijayo, baada ya kupata ushindi wa bao 1-0 kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, juzi.