Tuesday, 4 March 2014

Yanga wampa pesa Amissi Tambwe


 

YANGA wamemshitua straika wa Simba, Amissi Tambwe baada ya kumzingira, kuonyesha hisia zao kwa makali yake ya kucheka na nyavu halafu wakampooza na buku 10 akabaki anacheeka huku mashabiki wa timu yake wakiingiwa hofu.
Mashabiki hao walifanya tukio hilo baada ya mechi ya Ligi Kuu Bara kati ya Simba na Ruvu Shooting kwenye Uwanja wa Taifa juzi Jumapili, baada ya mchezaji huyo kufunga mabao mawili Simba ikishinda 3-2.
Mabao hayo yalimfanya Tambwe kutimiza mabao 19 kwenye msimamo wa wafungaji ambapo ameweka rekodi ya aina yake kwani katika miaka ya hivi karibuni hakuna mchezaji aliyefikisha mabao hayo.
Mashabiki hao waliosimama upande wa Jukwaa la Yanga, mechi hiyo ilipomalizika walipiga kelele wakiita jina la Tambwe ili wazungumze naye jambo na kumpongeza kwa makali yake na  alivyowafuata walimgombania na mmoja wao akampa buku 10 (Sh 10,000) akainyaka akaishia zake nje ya uwanja.
Mchezaji huyo aliwaacha mashabiki hao wakijadiliana huku wakionekana kufurahishwa na akili ya kuona goli aliyonayo straika huyo. Tambwe alipofuatwa na Mwanaspoti baada ya kuachana na mashabiki hao alionyesha kushangazwa na walichomfanyia Yanga kwani hakutarajia lakini hakutaka kuingia kiundani kwa kuhofia inaweza kumletea matatizo kwa viongozi wake na mashabiki.
Tambwe alisema: “Nashukuru na nafikiri wamevutiwa na mimi, siwezi kuzungumzia zaidi.” Pamoja na kucheza vizuri kwenye mchezo huo, Zdravko Logarusic alimtoa kwenye mechi hiyo zikiwa zimebaki dakika 18 na akasema alifanya hivyo kwa ajili ya kumlinda.
“Unajua nafanya hivi kwa sababu uwezo wake wa kufunga mabao mengi huwa ni kero kwa mabeki wa timu pinzani ambao huwa wanamwinda ili wamuumize na ndivyo nilivyoona, ndiyo maana nikamtoa,” alisema Logarusic.
“Si unajua kama watafanikiwa malengo yao ya kumuumiza akakaa nje atakuwa ameigharimu timu, Tambwe ni mchezaji mzuri na muhimu kwenye timu ukimkosa ni hatari.”
Awaambia mashabiki Simba
Tambwe amesema kitendo cha mashabiki kumshangilia yeye pekee baada ya mechi si kizuri kwani kinaweza kuigawa timu hiyo kongwe nchini. Katika mechi dhidi ya JKT Ruvu na Ruvu Shooting zilizochezwa Uwanja wa Taifa, Dar es Saalam, Tambwe alipokewa kwa shangwe na mashabiki wa Simba hadi lango kuu la kutokea uwanjani hapo ambapo huchukua bajaji na kuondoka.
Akizungumzia suala hilo Tambwe alisema, “Unajua ni vizuri kumpongeza mtu anapofanya vizuri ila pia mashabiki wanapaswa kukumbuka kuwa mimi si kitu nikiwa peke yangu, hii ni timu na mimi ni mfungaji tu.”
“Mashabiki wanapaswa kuelewa kuwa bila kazi kubwa inayofanywa na wachezaji wengine mimi nisingeweza kufunga, hivyo waishangilie timu kwa ujumla,” aliongeza Tambwe.

“Nina malengo ya kucheza soka la kulipwa nje ya Afrika Mashariki na pengine nje ya Afrika lakini unapotaka dili zikuangukie lazima uwe na kitu fulani tayari umeshakifanya hivyo kama straika ninahitaji kuwa na mabao ya kutosha.”
“Mimi kwa michezo sita iliyobaki nataka kuhakikisha, mitatu ijayo ninapata mabao sita na hiyo michezo mingine itakayosalia ni mipango ya Mungu tu.
“Nina mabao 19 na nikifikisha 25 nitakuwa nimejitangaza vya kutosha na kuzikaribisha timu nyingine kwa ajili ya kufanya kazi na mimi. Ninavyoongea na wewe DC Motema Pembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo inanihitaji,” alisema.