Tuesday, 4 March 2014

Mambo ya Ngassa yazidi kutikisa Afrika



 
Ngassa aliweka rekodi ya kufunga ‘hat trick’ mbili katika mechi mbili za hatua ya awali dhidi ya Komorozine de Domoni ya Comoro ambayo Yanga waliipata ushindi wa jumla ya mabao 12-2. 
MSHAMBULIAJI wa Yanga, Mrisho Ngassa bado anashikilia rekodi ya kufunga ‘hat trick’ mbili kwenye mechi za Ligi ya Mabingwa Afrika baada ya mechi za hatua ya kwanza ya michuano hiyo kushindwa kupata
‘hat trick’ yoyote.
Michezo 16 ya Ligi hiyo ilichezwa wikiendi iliyopita ikishuhudia washambuliaji wa timu hizo 32 wakishindwa kuivunja rekodi hiyo ya Ngassa hivyo kumwacha akiendelea kubakia kuwa kinara wa mabao 6 katika michuano hiyo.
Ngassa aliweka rekodi ya kufunga ‘hat trick’ mbili katika mechi mbili za hatua ya awali dhidi ya Komorozine de Domoni ya Comoro ambayo Yanga waliipata ushindi wa jumla ya mabao 12-2. Ngassa alifunga mabao matatu katika mechi ya kwanza Jijini Dar es Salaam ambayo Yanga ilishinda mabao 7-0, kabla ya kufanya hivyo tena mjini Mitsamiouli, Comoro wiki moja baadaye Yanga ilipopata ushindi wa mabao 5-2.
Kwa sasa Ngassa anafuatiwa na washambuliaji Mouhcine Iajour wa Raja Casablanca ya Morocco na Lamine Diawara wa Stade Malien ya Mali waliofunga hat trick moja kila mmoja.
Kingston Nkhatha wa Kaizer Chief pia ana mabao matatu aliyofunga katika mechi mbili tofauti.
Endapo Ngassa atafanikiwa kupata mabao mengine na kuchukua tuzo hiyo ya ufungaji bora wa ligi hiyo, atakua mchezaji wa kwanza kuweka rekodi hiyo katika historia ya soka la Tanzania.